Advertisements

Saturday, August 23, 2014

Profesa Mbilinyi afichua siri nzito

Aliyewahi kuwa Waziri wa Fedha, Profesa Simon Mbilinyi akifanya mahojiano na mwandishi wa gazeti hili, hayupo pichani, nyumbani kwake jijini Dar es Salaam.

Dar es Salaam. Aliyekuwa Waziri wa Fedha, Profesa Simon Mbilinyi amefichua siri na kueleza kwamba wakati alipochaguliwa kuiongoza wizara hiyo nchi ilikuwa imefilisika.
Hata hivyo, alisema kuwa kwa ushirikiano na rais wa wakati huo, aliweza kuimarisha uchumi ndani ya siku 365 alizofanya kazi.
Profesa Mbilinyi aliyeshika wadhifa huo katika Serikali ya Awamu ya Tatu iliyoongozwa na Rais Benjamin William Mkapa, alisema hayo kwenye mahojiano maalumu na gazeti hili nyumbani kwake Upanga, Dar es Salaam, ambapo alieleza hali ya uchumi ilivyo sasa ikilinganishwa na miaka 19 iliyopita.
Alisema wakati alipopewa jukumu la kuiongoza wizara hiyo mwaka 1995 na Rais Benjamin Mkapa, alikuta uchumi umetetereka kwa kiasi kikubwa, hata taifa kushindwa kukubalika na taasisi za fedha za kimataifa na wafadhili waliosusa kutoa misaada wala kuikopesha fedha.
“Mkapa aliniteua kuwa waziri wake wa fedha, lakini wakati ananikabidhi ofisi hiyo, hali ya uchumi ilikuwa ni mbaya sana. Nilikuta uchumi umetetereka, sababu hatukulipa madeni ya kimataifa, wakasusa. Kimsingi nchi ilifilisika, lakini hatukuweza kusema mbele ya wananchi,”alisema Profesa Mbilinyi na kuongeza:
“Nilikubali na kuanza kufanya kazi kama waziri tukishirikaina naye (Mkapa), katika mambo mbalimbali ili kuweka uchumi katika hali nzuri. Uhusiano baina ya Serikali na taasisi hizo za kimataifa pia nchi wafadhili haukuwa mzuri, kwa hiyo tukajitahidi kurudisha heshima yetu. Tulirudisha heshima na kukubali masharti machache ya msingi ya Shirika la Fedha Duniani(IMF) na Benki ya Dunia, ikiwamo suala la uanachama, uchumi ukaanza kufufuka.”
“Kwa kipindi hicho hatukuingia kwenye makubaliano mengine ya mikopo hadi baadaye sana. Kwa hiyo ndiyo ilikuwa njia ya kurudi kwa IMF na WB kwa kuzingatia hayo,”alifafanua Profesa Mbilinyi.
Baada ya muda kiasi alisema wakaanza tena kufanya makubaliano ya baina ya nchi mbili na kuanza tena kupata misaada hasa kutoka Korea Kaskazini, India, Japan na Urusi na baadaye uchumi ukaanza kuonekana unaweza kufufuka ndipo Benki ya Dunia ikarejea na makubaliano ya kawaida.
“Hata hivyo, sikukaa hapo muda mrefu. Nilifanya kazi zote ndani ya mwaka mmoja nikamaliza. Hapo tulishainua uchumi hadi ukakaa sawa, tulikuwa kwenye nafasi nzuri kiuchumi kama nchini nyingine wanachama wa Benki ya Dunia,”alisema.
Kiongozi huyo mkongwe wa masuala ya uchumi alisema, licha ya kuwa alifanya kazi kwa juhudi na bidii kwa ajili ya masilahi ya taifa katika Wizara ya Fedha, baadhi wa watu hawakuona jema katika hilo.
“Licha ya kuwa mambo yalienda vizuri, kipindi hicho cha mwaka mmoja nilijenga uadui na watu wengi kwani niliwazibia mianya ya ulaji. Hata hivyo, jambo hilo ndilo lililosababisha kuachia nafasi hiyo na kumwambia Mkapa:“Naenda kuendelea na ubunge wangu, mchague mwingine akusaidie katika masuala ya fedha,”alisema Mbilinyi na kuongeza kuwa hilo ni moja kati ya mambo yaliyoweka historia katika maisha yake ya kulitumikia taifa la Tanzania.
Profesa Mbilinyi ambaye pia amewahi kuwa mashauri wa kiuchumi wa Hayati Mwalimu Julius Nyerere, alisema baada ya uamuzi huo aliamua kujikita kwenye ubunge pekee.
“Wakati Mkapa aliponiteua kuwa waziri wake wa fedha nilikuwa mbunge wa Peramiho, hivyo baada ya mwaka mmoja na kama mwezi mmoja hivi nilipoamua kuachia wadhafa huo, nikawa mbunge kwa jimbo langu kwa miaka kumi, kabla ya kuacha kujihusisha na masuala ya kisiasa. Huo ndiyo ukawa mwisho na siasa zangu. Ilikuwa mwaka 2005,” alisema Profesa Mbilinyi.
Akilinganisha hali ya uchumi wakati alipokuwa waziri na sasa, Profesa Mbilinyi ambaye sasa anafanya shughuli za mshauri wa uchumi akiwa pia mkulima na mfugaji alisema kuwa kwa mtazamo wake mwenendo wa uchumi ni mzuri.
“Sasa hivi nadhani una matatizo ya kawaida, lakini tunaendelea vizuri. Kwa mwendo huu, nadhani tutafikia malengo ya kuwa kati ya mataifa yenye uchumi wa kati duniani ifikapo mwaka 2025, kama tukiendelea hivi ,” alisema Profesa Mbilinyi na kuongeza:
“Kwa gesi iliyogunduliwa, uwezekano wa kupatikana mafuta na madini, inatia imani kwamba tunaweza kufika mbali. Rais Kikwete awe wa mwisho kuiongoza Tanzania ikiwa katika hali ya umasikini. Lakini pia nampongeza Rais Kikwete kwa kufikisha uchumi wa nchi ulipo sasa.”
Kuteuliwa na Nyerere
Akizungumzia kuteuliwa kwake na Nyerere alisema: “Alikuwa mwalimu wangu nilipokuwa nasoma Shule ya Sekondari Pugu. Wakati anaondoka kwenda kuanza siasa mwaka 1955 alituacha pale. Nilimaliza shule 1956 nikawa nafanya kazi ya kuuza mafuta Sheli BP, Pugu.
Lakini wakati huo nilikuwa namsaidia Mwalimu kufundisha makada wa TANU ambao ni vijana.
Niliwafundisha hesabu na Kiingereza wakati wa usiku katika Mtaa wa Lumumba kwa sababu wakati ule watumishi wa Serikali walikuwa hawaruhusiwi kuingia kwenye siasa” alisema Profesa Mbilinyi.
Aliongeza: “Alipokuwa rais akakumbuka kuwa Mbilinyi yupo Chuo Kikuu na kwa vile nilikuwa nafundisha vijana wa TANU, basi akaniita mimi pamoja na Justine Rweyemamu tumsaidie kumsomea makaratasi yake ya uchumi.
Alikuwa anasema kuwa uchumi wake ni wa kisiasa, hivyo tukawa wasaidizi wake wa masuala ya uchumi pamoja na vijana wengine kama saba hivi.”

Alielezea kuwa alifanya kazi na Mwalimu Nyerere kwa maika minane na kwamba anamkumbuka kwa mambo mengi.
Mwananchi

2 comments:

Anonymous said...

Kila Rais anasema amepewa nchi ikiwa imefilisika... Mwinyi, Mkapa and muda si mrefu Kikwete. Hamuoni aibu?

Anonymous said...

Ustaadhi Mwinyi alikuwa hakusanyi kodi na rushwa ilikuwa Nnje Nnje...sasa unafikiri nchi ingepata wapi pesa.

Huyu wa sasa naye yuko kwenye biashara ya unga. Kazi kweli kweli kwa maustadhi wakishika nchi.